HOTELI ALIYOFUNGUA KIKWETE YAVUNJWA
Na Eliya Mbonea, Arusha
SAA 48 tu tangu Rais Jakaya Kikwete azindue Hoteli ya Kitalii ya Snow Crest huko Ngulelo mjini Arusha, Wakala wa Barabara nchini (TANROADS) wameivunja.
Jana saa 11.30 asubuhi, tingatinga la wakala hao lilifika hotelini hapo pembeni ya barabara ya Arusha – Moshi na kuvunja ukuta wa mbele na geti la hoteli kwa madai umejengwa ndani ya hifadhi ya barabara.
Hoteli hiyo ilizinduliwa Ijumaa iliyopita na Rais aliyeonyesha kuridhishwa na ramani ya hoteli hiyo pamoja na ujenzi wake.
Rais, katika mazungumzo hotelini hapo, alionyesha kukerwa na tabia ya wafanyakazi wazawa wanaoendekeza wizi na udokozi na kuwaogopesha wamiliki wa hoteli hivyo kuamua kuajiri wafanyakazi kutoka nje ya nchi.
Kikwete pia aliwapongeza wamiliki wa hoteli hiyo yenye vyumba 83.
MTANZANIA likiwa katika eneo la tukio lilishuhudia ukuta ambao awali ulikuwa umenakishiwa kwa taa na kupambwa kwa vimulimuli vya kukaribisha wageni hasa kipindi hiki cha sikukuu za mwishoni mwa mwaka ukiwa umepondwapondwa na katapila la TANROAD na kuharibu mandhari nzima ya eneo hilo.
Baadhi ya wafanyakazi wa hoteli hiyo walionekana wakiokota mabaki ya tofali za ukuta huo.
Mkurugenzi wa Hoteli hiyo, William Tarimo alisema kitendo hicho kinaonyesha kuwapo kwa chuki za kibiashara na kushangaa kwa nini ukuta huo uvunjwe wakati wageni kutoka ndani na nje ya nchi wakiwa bado wamepumzika.
“Ni chuki, ukitembea kutoka hapa hadi KIA utakuta nyumba nyingi tu zimesogea barabarani, lakini wametuoana sisi tu.
“Tulikuwa tumekubaliana kuwa kilichotakiwa kutolewa ni grill na si uharibifu wa eneo la kuegesha magari kama hivi. Tulikubaliana kuwa hiki tulichokiweka ni kwa muda tu,” alisema Tarimo.
Alisema uvunjaji huo umeharibu miundombinu kadhaa ya hoteli hiyo kama simu na umeme.
“Hizi ni chuki za kibiashara. Kama sisi wawekezaji wa ndani tunafanyiwa hivi hii ni hatari sana,” alisema Tarimo
Alisema ofisa wa TANROADS alishirikishwa wakati wa ujenzi wa uzio huo wa muda na hakukuwa na haja ya kubomoa vile na kuipa hasara ya mamilioni ya fedha hoteli hiyo.
Diwani wa Kata ya Baraa, Paul Laizer aliyefika eneo la tukio alisema ameshangazwa na uamuzi wa haraka haraka wa kuvunja uzio huo siku mbili tu tangu Rais aizindue.
“Si kitendo cha kiungwana kabisa. Ilipaswa kuwepo kwa mawasiliano ya kiungwana si namna hii. Wangejaribu hata kuheshimu uwepo wa raia wa nje au basi wangemuheshimu Rais,” alisema Diwani huyo.
.
Maoni
Jina
Barua Pepe